SERIKALI YAIHAKIKISHIA TBC KUTATUA CHANGAMOTO ZINAZOWAKABILI
Mgeni rasmi Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Jerry William Silaa akiwasili katika ukumbi wa Hazina, kufungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) na kupokelewa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) Stephen Kagaigai na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo Dkt. Ayub Rioba Chacha leo Septemba 20, 2024 jijini Dodoma.
Na Mwandishi Wetu, WHMTH, Dodoma
SERIKALI imelihakikishia Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) kwamba inafanya kila linalowezekana kuhakikisha shirika hilo linatekeleza majukumu yake muda wote, na itaendelea kutatua na kumaliza changamoto zote zinazolikabili, zikiwemo za kifedha, vifaa na raslimali watu.Ahadi hiyo ya serikali imetolewa Septemba 19, 2024 na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Jerry Silaa (Mb), wakati akifungua Kikao cha Pili cha Baraza la Wafanyakazi wa TBC kilichofanyika katika ukumbi wa Kambarage (Hazina) jijini Dodoma.
"Naomba niwahakikishie kuwa, serikali inafanya kila linalowezekana ili TBC itekeleze majukumu yake muda wote, wizara itahakikisha changamoto zote zinazowakabili zinatatuliwa kwa wakati kwani mkakati wa serikali ni kuhakikisha mnawezeshwa kifedha, vifaa na rasilimali watu ili kutekeleza dhima yake kwa umma wa watanzania," amesema Mhe.Silaa.
Mhe. Silaa amesema, serikali inatambua juhudi mbalimbali zinazofanywa na TBC kuhakikisha kunakuwa na fedha za kutosha na kwamba kwa kutambua changamoto za kifedha kwa shirika, wizara inasimamia kwa karibu mchakato wa kutungwa kwa sheria ya TBC, aliyosema pamoja na mambo mengine, itaiwezesha kupata vyanzo vya mapato vya uhakika, endelevu na toshelevu.
"Waraka wa sheria hii umeshasomwa kwa mara ya kwanza Bungeni na hatua inayofuata ni kupitishwa na Bunge baada ya kupata maoni ya wadau kama taratibu zinavyoelekeza," amesema Mhe. Silaa.
Aidha, ameipongeza TBC kwa maendeleo makubwa yaliyofikiwa ya kufunga mifumo ya TEHAMA katika miundombinu ya studio za redio na televisheni, upanuzi wa usikivu uliofikia asilimia 92 mwaka huu na maendeleo ya ujenzi wa makao makuu ya TBC eneo la Vikonje Dodoma uliofikia asilimia 26 hadi sasa.
Awali, akimkaribisha Waziri, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) Stephen Kagaigai amewashauri watanzania kufuatilia maudhui yanayotolewa na shirika hilo kwani ndicho chombo cha umma wa watanzania.
Naye, Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo Dkt. Ayub Rioba Chacha ameishukuru serikali kwa uwekezaji mkubwa uliofanywa unaowezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi mkubwa, licha ya changamoto ndogo ndogo ikiwemo ya upungufu wa watumishi wenye ujuzi kwani waliokuwepo wengi sasa wamefikia umri wa kustaafu.
Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Jerry William Silaa akiwa katika picha ya pamoja na makundi mbalimbali ya Wajumbe wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) kilichofanyika leo Septemba 20, 2024 katika ukumbi wa Hazina jijini Dodoma
Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Jerry William Silaa akiagana na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) Stephen Kagaigai na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo Dkt. Ayub Rioba Chacha mara baada ya kufungua Kikao cha Baraza la wafanyakazi wa TBC kilichofanyika leo Septemba 20, 2024 katika ukumbi wa Hazina jijini Dodoma.
No comments