Header Ads

ad

Breaking News

Mkataba wasainiwa kulindwa shoroba ya Kwakuchinja

Na Mwandishi Wetu, Babati

SERIKALI imesaini mkataba wa kulindwa kwa eneo la mapito ya wanyamapori (shoroba) la Kwakuchinja ambalo lipo kati kati ya hifadhi ya Taifa ya Tarangire na Hifadhi ya Taifa ya Ziwa Manyara, ili kuzuia uvamizi wa eneo hilo na kupunguza migogoro baina ya wanyamapori na binaadamu.

Katibu Tawala Msaidizi wa Mkoa wa Manyara (Uchumi na Uzalishaji), Faraja Ngerageza akizungumza na waandishi wa habari, baada ya kusainiwa mkataba huo, baina ya Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Idara ya Wanyamapori na Taasisi ya Chem Chem, amesema ushoroba huo utatunzwa kutokana na umuhimu wake.

Ngerageza amesema Ushoroba wa Kwakuchinja una manufaa makubwa ya kiuchumi kwa mkoa wa Manyara na Taifa kwa ujumla hivyo lazima ilindwe na kutunzwa.

"Sisi mkoa tayari tumekamilisha taratibu zetu za kuhifadhiwa Shoroba hii, ili kuendelezwa shughuli za uhifadhi na Utalii na tayari eneo limepimwa na mipaka yote imewekwa," amesema

Amesema mkoa kwa sasa unaendelea kutoa elimu kwa wananchi ambao wanaishi jirani na eneo hilo kufanyashughuli ambazo ni rafiki kwa shughuli za uhifadhi na Utalii.

Afisa Wanyamapori Mkoa Manyara, Felix Mwasenga amesema eneo la kilomita 137 ambalo ni Shoroba kwa Kuchinjwa tayari limebainishwa.

Mwasenga amesema eneo hilo linapatikana katika vijiji vya Vilima Vitatu, Kakoi, Minjingu na Olasiti.

Hata hivyo amesema katika eneo hilo asilimia 20.9 lipo katika vijiji na asilimia 116 lipo katika Hifadhi ya Jamii ya Burunge WMA.

Awali, akizungumza wakati wa kusainiwa mkataba huo, Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Wanyamapori, Eligi Kimario amesema mkataba huo umesainiwa wakati muafaka ili kupunguza migogoro baina ya wanyamapori na binaadamu katika eneo hilo.

Kimario amesema ushoroba huu unahifadhiwa kuruhusu wanyamapori kuvuka kutoka Hifadhi na Tarangire na kwenda Hifadhi ya Manyara na kurudi bila kusababisha migogoro.

Amesema kumekuwepo na migogoro katika eneo hilo hasa baada ya baadhi ya wananchi kujenga nyumba na kulima eneo la mapito ya wanyamapori.

Amesema katika mkataba huo,Taasisi ya Chem Chem inatarajiwa kuwajengea uwezo wa masuala ya uhifadhi watumishi ambao wanalinda ushoroba huo na pia kusaidia kulindwa.

Katibu wa Taasisi ya Chem Chem , Charles Sylivester amasema katika mkataba wanatarajia kushirikiana na serikali kulinda na kuhifadhi shoroba ya kwakuchinja.

Anasema mkataba huo, utakuwa na miaka mitano na unaweza kuendeleza na utasaidia uhifadhi wa eneo hilo muhimu kwa sekta ya utalii na uhifadhi nchini.

Viongozi mbalimbali wameshiriki utiaji saini mkataba huu mjini Babati wakiwepo viongozi wa Burunge WMA na viongozi wa taasisi za uhifadhi.






No comments