ISLAND OF PEACE YAPIGANIA KILIMO IKOLOJIA HAI KUDHIBITI UDUMAVU, UNENE
Na Mwandishi Wetu
PAMOJA na Tanzania kujitosheleza kwa chakula kwa asilimia
120, imeelezwa bado kuna changamoto ya lishe kwa jamii, ambapo takwimu za
Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) 2020, zikionesha asilimia 34 ya
watoto nchini wanaabiliwa na udumavu.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Island of
Peace (IDP) Tanzania, Ayesiga Buberwa wakati wa dhifa ya kitaifa ya chakula cha
usiku cha asili iliyoandaliwa na shirika hilo na wadau wengine wa kilimo
ikolojia nchini.
Alisema takwimu za WFP zinaonesha asilimia 34 ya watoto
wenye miaka chini ya miaka mitano wanakabiliwa na udumavu, hivyo kama kuna
mambo ya kuangalia kwa umakini kwa sasa ni kuhusu afya ya watu.
Ayesiga alisema anavyosema asilimia 34 ya watoto ni sawa na
kusema kati ya watoto 100 watoto 34 wana utapiamlo wa udumavu na kwamba udumavu
huo hauhusu mahindi wala wanyama, bali ni mustakabali wa watu.
Mkurugenzi huyo alisema taarifa hiyo ya WFP ilisema pia
asilimia 62 ya vijana wenye miaka 15 hadi 18 wana udumavu, hivyo ni wazi kuwa
udumavu ni changamoto kubwa nchini.
“Takwimu zinaonesha
Tanzania inajitosheleza kwa chakula kwa asilimia 120, jambo ambalo ni la
kupongezwa, ila kuna changamoto kubwa ya udumavu wa watoto wetu na rika la
kati, tunapaswa kukabiliana nayo kwa pamoja kwa kusisitiza ulaji wa vyakula vya
asili,” alisema.
Alisema kuna jitihada zinachukuliwa na wadau mbalimbali
katika kukabiliana na changamoto hiyo, ila ameomba nguvu kubwa kuongezeka hasa
katika kuhamasisha ulaji wa vyakula asili ambayo utafiti utafiti umeonesha vina
faida.
“Sijasema changamoto
za ukosefu wa damu na madini kwa mama wajawazito na wanaonyonyesha, vyote hivyo
ukiviangalia, ikiwemo njaa iliyofichika, udumavu na utapiamlo, vyote hivyo
vinasababishwa na nini tunakula, tunakula saa ngapi, kwa namna gani na
kuviandaa aje,” alisema.
Ayesiga alisema changamoto nyingine ya kula vyakula visivyo
vya asili ni uzito uliokithiri kuongezeka.
Mkurugenzi mkazi huyo alisema changamoto hizo zinapaswa
kuwafikirisha viongozi wa hali ya juu, ili kuhakikisha tatizo hilo
linapunguzwa, iwe kwa kutunga sera au kufanya utafiti wa kina kupitia taasisi
za kitafiti kama Kituo cha Utafiti Tanzania (TARI), Chuo Kikuu cha Nelson
Mandela na wengine.
Alisema iwapo kila mdau atafanyia kazi eneo lake kwa kina,
upo uwezekano wa kuifanya jamii ifurahie chakula cha asili na kuondoa
changamoto ya njaa iliyofichika.
“Vyakula vya asili vinalenga kutunza utamaduni wetu, hivyo
sisi kama Islands of Peace tunajitahi kwa upande wetu kuikomboa jamii ya
kitanzani katika eneo la lishe,” alisema
Ayesiga alisema katika dhifa hiyo ambayo imebeba na kauli
mbiu ya ‘Kuboresha Lishe kupitia Vyakula Asili na Kitamaduni’ wameshirikiana
kuanda na Wizara ya Kilimo, Pelum-Tanzania, Shirikisho la Vyama vya Wakulima na
Wafugaji Tanzania (SHIWAKUTA) na We Effect.
Akizungumza katika hafka hiyo Mgeni rasmi Waziri Mkuu
mstaafu, Mizengo Pinda amezitaka tasisi zinazohamasisha kilimo ikolojia hai
kushirikisha viongozi wa dini, serikali na shule ili uelewa uweze kufikia watu
wengi.
“Mimi nimetafakari
sana namna ya kukabiliana na changamoto hii ya udumavu ambayo imetajwa napenda
kutumia nafasi hii kuziomba taasisi zote za kupigania kilimo ikolojia hai
weweke mkazo kwa viongozi wa dini, serikali za mitaa na shuleni, tutaweza
kugusa jamii kubwa,” alisema.
Alisema watendaji wa serikali wana nafasi kubwa ya kusaidia
jamii kuondokana na udumavu, kwani kwa hali ilivyo sasa mtu anayekula
mbogamboga anaonekana hana akili, kumbe wasio kula ndi wana tatizo.
Waziri mkuu huyo mstaafu alisema ni vema Wizara ya Kilimo,
Afya, Fedha na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikal za Mitaa (TAMISEMI),
ziweze kukutana na kujadiliana namna ya kukabiliana na changamoto ya udumavu na
kueleza nini cha kufanya kwa maslahi ya nchi.
Pinda alisema nchi ya Tanzania ambayo ina ardhi nzuri, mvua
za kutosha ni aibu kuwa na zaidi ya watoto milioni 3.4 kuwa na udumavu, hivyo
ni lazima viongozi wote hasa wenye uwezo kuchukua hatua ili kuokoa taifa hili.
“Inawezekana watendaji wanatuangusha, ila sisi viongozi
ambao tumebahatika kuwa na maisha bora tumesababisha hali hii, ni wakati wa
kubadilika na kuiambia jamii faida ya kula mbogamboga kwa mwanadamu,” alisema.
Waziri mkuu huyo mstaafu alisema hakuna sababu ya Tanzania
kutamba kuwa katika uchumi wa kati wakati watu wake ni wadumavu.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde
alisema uamuzi wa IDP kuandaa dhifa hiyo ya chakula asili unapaswa kuungwa
mkono kwa kuwa unaenda kukomboa wananchi.
Alisema serikali inatambua kazi kubwa ambayo inafanywa na
taasisi zinazopigania kilimo ikolojia na ndio maana katika bajeti wametenga
fedha za ruzuku katika eneo hilo na ameahidi wataendelea kukiunga mkono kilimo
hicho.
“Tumejipanga kuendelea kilimo ikolojia hai ili kiwe na tija,
kama kilivyo kilimo kingine, kwani ushihidi unaonesha kina faida kiafya na
kiuchumi,” alisema.
Alisema serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu
Hassan imetenga fedha nyingi kwenye kilimo, hali ambayo imesababisha sekta hiyo
kuwa ya tatu kwa kuchangia fedha za kigeni.
No comments