Header Ads

ad

Breaking News

WATU 310 WAPIMA MOYO SIKU YA SHINIKIZO LA JUU LA DAMU DUNIANI


Mkurugenzi wa tiba wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Tatizo Waane akizungumza na wananchi waliofika katika Hospitali ya JKCI Dar Group wakati wa Kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services iliyofanyika kwa siku mbili katika kuadhimisha siku ya Shinikizo la juu la damu duniani inayoadhimishwa kila ifikapo Mei 17.

Na Mwandishi Maalumu, Dar es Salaam

WATU 310 wakiwemo watu wazima 264 na watoto 46 wamejitokeza kufanya uchunguzi na vipimo vya magonjwa yasiyoambukiza ya shinikizo la damu, sukari na moyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Hospitali ya JKCI Dar Group.

Upimaji huo umefanyika kwa siku mbili katika kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services wakati wa maadhimisho ya siku ya shinikizo la juu la damu duniani inayoadhimishwa kila ifikapo Mei 17.

Akizungumza wakati wa kilele cha siku ya moyo duniani kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge, Mkurugenzi wa Tiba wa JKCI Dkt. Tatizo Waane alisema kati ya watu wazima 264 waliofanyiwa uchunguzi katika kambi hiyo watu 43 sawa na asilimia 16 wamekutwa na magonjwa mbalimbali ya moyo.

Dkt. Waane alisema takribani asilimia 30 ya vifo vyote duniani vinatokana na magonjwa ya moyo hususani ugonjwa wa shinikizo la juu la damu hivyo kuwataka wananchi kuwa na mfumo bora wa maisha kuzuia magonjwa hayo.

“unapokutwa na tatizo la shinikizo la juu la damu kuna uwezekano wakupata athari mbalimbali katika viungo vya mwili kama vile moyo kushindwa kufanya kazi, kupata kiharusi, pamoja na matatizo ya figo”, alisema Dkt. Waane

Dkt. Waane alisema watu wakiwa na mazoea yakupima afya watakuwa na nafasi nzuri ya kujijua na kujilinda ili wasipate magonjwa yasiyoambukiza na kama tayari wameshayapata wataweza kujilinda ili magonjwa hayo yasiwasababishie changamoto nyingine.

Kwa upande wake daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Hospitali ya Dar Group Eva Wakuganda alisema katika upimaji huo watoto 46 wamefanyiwa kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiography – ECHO).

Dkt. Eva alisema watoto 12 sawa na asilimia 26 wamekutwa na matatizo mbalimbali ya moyo ikiwemo matundu, hitilafu katika milango ya moyo pamoja na moyo kutanuka.

“Baadhi ya watoto tuliowafanyia uchunguzi wapo ambao walishagundulika kuwa na matatizo ya moyo hapo awali lakini kutokana na hali ya maisha wakaona ni vyema kutumia nafasi hii kuangalia maendeleo yao na kupata dawa bila gharama”, alisema Dkt. Eva

Naye mwananchi aliyepatiwa huduma katika kambi hiyo Theresia Mjange ameishukuru Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kwa kuwajali wananchi na kuwapatia huduma bila gharama ili waweze kuchunguza afya zao.

Theresia alisema amefika Hospitali ya JKCI Dar Group kwaajili ya matatizo ya miguu lakini baada ya kuona kuna huduma nyingine za upimaji wa magonjwa ya moyo akaamua kushiriki katika zoezi la kupima moyo wake ili aweze kujijua.

“Nimefika hapa nimepata huduma vizuri bila ya usumbufu nimeweza kumuona daktari nikapimwa moyo baada ya hapo nikamuona mtaalamu wa lishe na mwisho nikapata dawa bure”, alisema

Siku ya shinikizo la juu la damu duniani uadhimishwa kila ifikapo Mei 17 ambapo mwaka huu kauli mbiu inasema “Pima shinikizo lako la damu kwa usahihi, tibu au zuia, uishi maisha marefu.”

Afisa Lishe wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Husna Faraji akimuelimisha mwananchi kuhusu lishe bora wakati wa Kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services iliyofanyika kwa siku mbili katika Hospitali ya JKCI Dar Group kuadhimisha siku ya Shinikizo la juu la damu duniani inayoadhimishwa kila ifikapo  Mei 17.


 Mteknolojia maabara wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Hospitali ya JKCI Dar Group Emmanuel Mapula akiwagawia vipeperushi vinavyoelezea ugonjwa wa shinikizo la damu wananchi waliojitokeza wakati wa Kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services iliyofanyika kwa siku mbili katika kuadhimisha siku ya Shinikizo la juu la damu duniani inayoadhimishwa kila ifikapo Mei 17.

Wataalamu wa afya wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Hospitali ya JKCI Dar Group wakiendelea kutoa huduma wakati wa Kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services iliyofanyika kwa siku mbili katika taasisi hiyo kuadhimisha siku ya Shinikizo la juu la damu duniani inayoadhimishwa kila ifikapo Mei 17.

Afisa Lishe wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Hospitali ya JKCI Dar Group Stanley Dickson akimuelimisha mwananchi kuhusu lishe bora wakati wa Kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services iliyofanyika kwa siku mbili katika Hospitali ya JKCI Dar Group kuadhimisha siku ya Shinikizo la juu la damu duniani inayoadhimishwa kila ifikapo Mei 17.

Mfamasia kutoka kampuni ya dawa za binadamu ya Microlabs Ltd. Festus Asenga akimpatia dawa mwananchi aliyepatiwa huduma katika Kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services iliyofanyika kwa siku mbili katika Hospitali ya JKCI Dar Group wakati wa kuadhimisha siku ya Shinikizo la juu la damu duniani inayoadhimishwa kila ifikapo Mei 17.

Mwananchi aliyefika katika kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services Angel Mallya akiuliza maswali wakati wa kilele cha siku ya shinikizo la juu la damu duniani iliyofanyika kwa siku mbili katika Hospitali ya JKCI Dar Group na kumaliza leo jijini Dar es Salaam. Picha zote na JKCI

No comments