WATU 310 WAPIMA MOYO SIKU YA SHINIKIZO LA JUU LA DAMU DUNIANI
Mkurugenzi wa tiba wa Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Tatizo Waane akizungumza na wananchi waliofika
katika Hospitali ya JKCI Dar Group wakati wa Kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia
Suluhu Hassan Outreach Services iliyofanyika kwa siku mbili katika kuadhimisha
siku ya Shinikizo la juu la damu duniani inayoadhimishwa kila ifikapo Mei 17.
Na Mwandishi Maalumu, Dar es Salaam
WATU 310 wakiwemo watu
wazima 264 na watoto 46 wamejitokeza kufanya uchunguzi na vipimo vya magonjwa
yasiyoambukiza ya shinikizo la damu, sukari na moyo katika Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete Hospitali ya JKCI Dar Group.
Upimaji huo umefanyika kwa siku mbili
katika kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services wakati
wa maadhimisho ya siku ya shinikizo la juu la damu duniani inayoadhimishwa kila
ifikapo Mei 17.
Akizungumza wakati wa kilele cha siku
ya moyo duniani kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge, Mkurugenzi wa Tiba wa JKCI Dkt. Tatizo Waane
alisema kati ya watu wazima 264 waliofanyiwa uchunguzi katika kambi hiyo watu
43 sawa na asilimia 16 wamekutwa na magonjwa mbalimbali ya moyo.
Dkt. Waane alisema takribani asilimia
30 ya vifo vyote duniani vinatokana na magonjwa ya moyo hususani ugonjwa wa
shinikizo la juu la damu hivyo kuwataka wananchi kuwa na mfumo bora wa maisha
kuzuia magonjwa hayo.
“unapokutwa na tatizo la shinikizo la
juu la damu kuna uwezekano wakupata athari mbalimbali katika viungo vya mwili
kama vile moyo kushindwa kufanya kazi, kupata kiharusi, pamoja na matatizo ya
figo”, alisema Dkt. Waane
Dkt. Waane alisema watu wakiwa na
mazoea yakupima afya watakuwa na nafasi nzuri ya kujijua na kujilinda ili
wasipate magonjwa yasiyoambukiza na kama tayari wameshayapata wataweza
kujilinda ili magonjwa hayo yasiwasababishie changamoto nyingine.
Kwa upande wake daktari bingwa wa
magonjwa ya moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Hospitali ya Dar
Group Eva Wakuganda alisema katika upimaji huo watoto 46 wamefanyiwa kipimo cha
kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiography – ECHO).
Dkt. Eva alisema watoto 12 sawa na
asilimia 26 wamekutwa na matatizo mbalimbali ya moyo ikiwemo matundu, hitilafu
katika milango ya moyo pamoja na moyo kutanuka.
“Baadhi ya watoto tuliowafanyia
uchunguzi wapo ambao walishagundulika kuwa na matatizo ya moyo hapo awali
lakini kutokana na hali ya maisha wakaona ni vyema kutumia nafasi hii kuangalia
maendeleo yao na kupata dawa bila gharama”, alisema Dkt. Eva
Naye mwananchi aliyepatiwa huduma
katika kambi hiyo Theresia Mjange ameishukuru Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
kwa kuwajali wananchi na kuwapatia huduma bila gharama ili waweze kuchunguza
afya zao.
Theresia alisema amefika Hospitali ya
JKCI Dar Group kwaajili ya matatizo ya miguu lakini baada ya kuona kuna huduma
nyingine za upimaji wa magonjwa ya moyo akaamua kushiriki katika zoezi la
kupima moyo wake ili aweze kujijua.
“Nimefika hapa nimepata huduma vizuri
bila ya usumbufu nimeweza kumuona daktari nikapimwa moyo baada ya hapo
nikamuona mtaalamu wa lishe na mwisho nikapata dawa bure”, alisema
Siku ya shinikizo la juu la damu duniani uadhimishwa kila ifikapo Mei 17 ambapo mwaka huu kauli mbiu inasema “Pima shinikizo lako la damu kwa usahihi, tibu au zuia, uishi maisha marefu.”
Afisa Lishe wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Husna Faraji akimuelimisha mwananchi kuhusu lishe bora wakati wa Kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services iliyofanyika kwa siku mbili katika Hospitali ya JKCI Dar Group kuadhimisha siku ya Shinikizo la juu la damu duniani inayoadhimishwa kila ifikapo Mei 17.
Mteknolojia maabara wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Hospitali ya JKCI Dar Group Emmanuel Mapula akiwagawia vipeperushi vinavyoelezea ugonjwa wa shinikizo la damu wananchi waliojitokeza wakati wa Kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services iliyofanyika kwa siku mbili katika kuadhimisha siku ya Shinikizo la juu la damu duniani inayoadhimishwa kila ifikapo Mei 17.
Wataalamu wa afya wa Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete Hospitali ya JKCI Dar Group wakiendelea kutoa huduma wakati wa
Kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services iliyofanyika
kwa siku mbili katika taasisi hiyo kuadhimisha siku ya Shinikizo la juu la damu
duniani inayoadhimishwa kila ifikapo Mei 17.
Afisa Lishe wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete Hospitali ya JKCI Dar Group Stanley Dickson akimuelimisha mwananchi
kuhusu lishe bora wakati wa Kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan
Outreach Services iliyofanyika kwa siku mbili katika Hospitali ya JKCI Dar
Group kuadhimisha siku ya Shinikizo la juu la damu duniani inayoadhimishwa kila
ifikapo Mei 17.
Mfamasia kutoka kampuni ya dawa za
binadamu ya Microlabs Ltd. Festus Asenga akimpatia dawa mwananchi aliyepatiwa
huduma katika Kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services
iliyofanyika kwa siku mbili katika Hospitali ya JKCI Dar Group wakati wa
kuadhimisha siku ya Shinikizo la juu la damu duniani inayoadhimishwa kila
ifikapo Mei 17.
Mwananchi aliyefika katika kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services Angel Mallya akiuliza maswali wakati wa kilele cha siku ya shinikizo la juu la damu duniani iliyofanyika kwa siku mbili katika Hospitali ya JKCI Dar Group na kumaliza leo jijini Dar es Salaam. Picha zote na JKCI
No comments