NAIBU WAZIRI KIKWETE AUSIFIA MFUMO WA USAILI KIDIGITALI
Na Mwandishi Wetu
NAIBU Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete amesema kitendo cha Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma kuanza kutumia rasmi mfumo wa usaili wa kidigitali utamwezesha mwombaji kusailiwa eneo alilopo, badala ya kusafiri umbali mrefu.
Kikwete amesema hatua hiyo itapunguza gharama kwa Serikali na kwa wanaosailiwa, hivyo ni mafanikio makubwa ya Serikali ya Awamu ya Sita chini inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweka uwazi kwenye mchakato wa kutoa ajira.
Naibu Waziri Kikwete ameyasema hayo mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam, baada ya kushuhudia wasailiwa wa kada ya tehama wakifanya usaili huo katika Chuo Kikuu cha St. Joseph , ikiwa ni moja ya kituo cha usaili wa mchujo unaofanyika kidigitali katika kila mkoa nchi nzima, ikiwa ni usaili wa kwanza tangu mfumo huo ulipozinduliwa hivi karibuni
Amesema mfumo huo umeanza kutumika wakati sahihi wakati Rais Dkt. Samia akiendelea na jitihada za kuimarisha uwazi na kuepuka upendeleo katika suala la utoaji ajira serikalini.
Amesema vituo 32 nchi nzima vimeendesha usaili huo uliowahusiah jumla ya wasailiwa 2325 wamepata fursa ya kufanya usaili huo pasipo kulazimika kusafiri umbali mrefu
Amesema vituo 32 vilifanyika usaili huo unaowashirikisha watahiniwa kutokaq Tanzania Bara na Visiwani, ambapo kwa Mkoa wa Dar es Salaam ulikuwa na vituo vinne kutokana na idadi kubwa ya wasailiwa waliokuwa wameomba.
Naibu Waziri Kikwete amesema ajira ni maisha ya watu, hivyo mchakato huo umefungua ukurasa mpya wa kukuza uwazi na uadilifu katika kuondoa malalamiko kwa wale ambao wanatafuta ajira serikalini.
Amesema mfumo huo mbali ya kusaidia kupunguza gharama za wasailiwa ambao walikuwa wakilalamika kusafiri umbali mrefu kwenda kwenye kituo cha usaili kwa kutumia muda mwingi na gharama kubwa, wakati huu wamesailiwa mahali walipo na kisha kuendelea kufanya shughuli nyingine za kujiingizia kipato.
Mkuu wa Idara ya Tehama kutoka Sekretariet ya Ajira katika Utumishi wa Umma, Mhandisi Samweli Tanguye amesema mfumo huo baada ya wasailiwa hao kumaliza kufanya mchujo watapata matokeo yao siku hiyo hiyo tofauti na ilivyokuwa mwanzo, ambapo matokeo yalikuwa yakichukua zaidi ya siku tatu.
Amesema mfumo huo unatoa nafasi kwa wasailiwa ambao wanafanya usaili zaidi ya mmoja ndani ya siku moja kuwa wigo wa kufanya usaili mwingine siku hiyo hiyo kwa saa tofauti, awali haikuwa rahisi.
Msailiwa wa kada ya Tehama, Juma Ali amepongeza ujio wa mfumo huo wa usaili wa kidijitali, huku akisema licha ya kumpunguzia gharama ya kusafiri hadi jijini Dodoma, lakini amepata fursa ya kuendelea kufanya shughuli nyingine mara baada ya kumaliza usaili wake.
Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete akishuhudia wasailiwa wa kada ya Tehama wakiendelea na usaili katika Chuo Kikuu cha St. Joseph, ikiwa ni moja ya kituo cha usaili wakifanya usaili wa mchujo unaofanyika kidigitali katika kila mkoa nchi nzima. Huo ni usaili wa kwanza tangu mfumo huo ulipozinduliwa hivi karibuni.
Baadhi ya wasailiwa wa kada ya Tehama wakiendelea na usaili katika Chuo Kikuu cha St. Joseph ikiwa ni moja ya kituo cha usaili kidigitali katika kila mkoa nchi nzima, ikiwa ni usaili wa kwanza tangu mfumo huo ulipozinduliwa hivi karibuni.
No comments