Header Ads

ad

Breaking News

JKCI kuokoa shilingi milioni 500, wagonjwa wa moyo 15 kutibiwa nchini

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu kambi maalumu ya upasuaji wa moyo inayofanywa na wataalamu wa afya wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao kutoka Shirika la Cardiostart International la nchini
Marekani. Kambi hiyo maalumu ya siku tano imeanza leo kwa mafunzo ya siku moja kwa wataalamu wa afya wa JKCI.


Na Mwandishi Maalumu, Dar es Salaam

TAASISI ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imeweza kuokoa kiasi cha shilingi milioni 500 ambazo Serikali ingeweza kutumia kuwapeleka wagonjwa wa moyo 15 nje ya nchi watakaotibiwa katika kambi maalumu ya upasuaji wa moyo na mishipa ya damu inayofanywa na taasisi hiyo.

Kambi hiyo maalumu ya siku tano inafanywa na wataalamu wa afya wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao kutoka Shirika la Cardiostart International la nchini Marekani kwa wagonjwa wa moyo na mishipa ya damu wanaohitaji matibabu ya upasuaji.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema Shirika la Cardiostart International limeanza kushirikiana na JKCI tangu mwaka 2019 ambapo hadi sasa wameshafanya kambi maalumu za matibabu ya moyo tano.

Aidha Dkt. Kisenge alisema sambamba na kutoa huduma za matibabu shirika hilo pia limeweza kutoa vifaa tiba kwa wagonjwa wa upasuaji wa moyo wanaotibiwa JKCI vyenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 200.

“Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ametengeneza mahusiano mazuri na nchi mbalimbali, mahusiano ambayo yanatuwezesha kupata wataalamu kutoka nchi tofauti kufika JKCI kwaajili ya kubadilishana ujuzi pamoja na kutoa huduma kwa wagonjwa wa moyo tunaowahudumia,” alisema Dkt. Kisenge.

Kwa upande wake Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu kwa watoto na watu wazima kutoka Shirika la Cardiostart International la nchini Marekani Prof. Aubyn Marath alisema JKCI haijarudi nyuma hata baada ya changamoto ya ugonjwa wa UVIKO 19 ulioiyumbisha dunia bado taasisi hiyo imeendelea kukuwa upande wa wataalamu wabobezi, huduma za kibingwa na uwezo wa kuokoa maisha ya wagonjwa.

Prof. Aubyn alisema shirika la Cardiostart International limekuwa likiunganisha nguvu ya wataalamu wote wa afya wanaofanya kazi katika chumba cha upasuaji wa moyo kuhakikisha kuwa ushirikiano katika kutoa huduma kwa wagonjwa unafanyika kwa kiwango cha hali ya juu kuokoa maisha.

“Wataalamu wa JKCI mmendelea kuonyesha utalamu wenu, uadilifu na kujitoa kwenu kuhakikisha kuwa huduma hizi za matibabu ya moyo zinaendelea kukuwa hapa Tanzania, nawapongeza sana kwa hilo”, alisema Prof. Aubyn.

Naye, daktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu kwa watu wazima wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Evarist Nyawawa alisema Prof. Aubyn kutoka Shirika la Cardiostart International amekuwa akiwawezesha wataalamu wa JKCI kutoa huduma za upasuaji mkubwa wa moyo na kupandikiza mishipa ya damu tangu kuanzishwa kwa matibabu hayo.

Dkt. Nyawawa alisema mbali na kutoa mafunzo ya upasuaji kwa wataalamu wa JKCI Prof. Aubyn aliweza kutafuta vyuo mbalimbali katika nchi tofauti na pale nafasi ilipopatikana aliwaunganisha wataalamu wa afya wa JKCI kupata mafunzo katika vyuo hivyo.

“Mimi ni mmoja wa wataalamu wa JKCI ambaye Prof. Aubyn aliniunganisha na chuo kilichopo nchini Brazil kupata mafunzo kupitia program zake za mafunzo ya upasuaji wa moyo na mishipa ya damu”, alisema Dkt. Nyawawa.

Dkt. Nyawawa alisema Cardiostart International imekuwa ikitoa ushirikiano na JKCI kuwaunganisha wataalamu mbalimbali duniani kufanya kambi za upasuaji wa moyo na JKCI.

 Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo kwa watoto na watu wazima kutoka Shirika la Cardiostart International la nchini Marekani Prof. Aubyn Marath akielezea mafanikio ya ushirikiano baina na JKCI na Cardiostart International wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu kambi maalumu ya siku tano inayofanywa na wataalamu hao katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu kwa watu wazima kutoka Shirika la Cardiostart International la nchini Marekani Prof. Gustavo Knop akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu kambi maalumu ya siku tano ya upasuaji wa moyo inayofanywa na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na Cardiostart International. Kambi hiyo maalumu imeanza leo ambapo wataalamu hao wameanza na mafunzo ya siku moja yatakayofuatiwa na kambi ya upasuaji wa moyo.

Baadhi ya watalaamu wa afya wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao kutoka Shirika la Cardiostart International la nchini Marekani wakisikiliza wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu kambi maalumu ya siku tano inayofanywa na wataalamu hao kuanzia leo tarehe 11 Machi hadi Ijumaa 15 Machi 2024.

Baadhi ya watalaamu wa afya wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao kutoka Shirika la Cardiostart International la nchini Marekani wakisikiliza wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu kambi maalumu ya siku tano inayofanywa na wataalamu hao kuanzia leo tarehe 11 Machi hadi Ijumaa 15 Machi 2024.Picha zote na Khamis Mussa.

No comments