Header Ads

ad

Breaking News

DAR ES SALAAM KUPIMA MOYO MACHI 2,3,2024

Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya JKCI Dar Group Idd Lemmah
akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kambi maalumu ijulikanayo kama, Dkt. Samia Suluhu Hassan tiba mkoba itakayofanyika Machi 2 na 3,2024 katika viwanja vya hospitali hiyo ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha siku ya wanawake duniani.


Mwandishi Maalumu, Dar es Salaam

TAASISI ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group kuadhimisha siku ya wanawake duniani kwa kufanya kambi maalumu ya upimaji na matibabu ya magonjwa ya moyo kwa wananchi.

Kambi hiyo ya siku mbili itafanyika katika viwanja vya Hospitali ya JKCI Dar Group Machi 2 na 3, 2024 kwa kufanya uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo kwa watoto na watu wazima.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya JKCI Dar Group, Idd Lemmah alisema upimaji huo unafanyika kupitia kambi maalumu ijulikanayo kama Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tiba mkoba iliyolenga kuwafikishia watanzania huduma za matibabu karibu.

“Tunawakaribisha watanzania mjitokeza, hususani watu  wanaoizunguka Hospitali hii wa Tazara na Temeke mfike katika siku hizi mbili mchunguze afya zenu,” alisema Lemmah.

Kwa upande wake Kaimu mkuu wa huduma za tiba wa Hospitali ya JKCI Dar Group, Dkt. Eva Wakuganda alisema kupitia kambi hiyo wananchi watapata fursa ya kutibiwa na wataalamu wa afya mabingwa wa magonjwa ya moyo.

Dkt. Eva ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto alisema wanawake wa JKCI Dar Group wameona umuhimu wa kuadhimisha siku ya wanawake duniani kwa kutoa huduma za matibabu ya moyo kwasababu wagonjwa wengi wamekuwa wakichelewa kufika hospitali kwaajili ya kupata matibabu.

“Kila watoto 100 wanaozaliwa mtoto mmoja uzaliwa na magonjwa ya moyo lakini bahati mbaya hawafiki hospitali mapema kwaajili ya kupatiwa matibabu hivyo kupitia kambi zetu za matibabu tunawatambua mapema na kuwapa huduma mapema,” alisema Dkt. Eva.

Dkt. Eva alisema kupitia kambi hiyo wananchi hupata elimu ya lishe na elimu ya kutambua magonjwa ya moyo hivyo kuwapa nafasi kujilinda na magonjwa hayo na pale wanapoyapata kuweza kuona dalili zake mapema hivyo kuwahi hospitali.


“Dalili za magonjwa ya moyo kwa watoto ni pamoja na kubadilika rangi kuwa wa bluu kwenye midomo na vidole, kushindwa kupumua vizuri, kutokuongezeka uzito, mapigo ya moyo kwenda mbio, kuchoka na kutokwa na jasho mara kwa mara”, alisema Dkt. Eva.

Naye, mwakilishi wa umoja wa wanawake Hospitali ya JKCI Dar Group Debora Mkemwa alisema wanawake wa Hospitali hiyo wameona umuhimu wa kuadhimisha siku ya wanawake duniani kwa kutoa huduma za matibabu ya moyo kwa wananchi kwani wanawake ndio nguzo ya kujenga familia bora.

“Wanawake ni msingi wa kuhakikisha familia zetu zinakuwa bora na imara kama ambavyo kauli mbiu ya siku ya wanawake duniani ya mwaka huu inavyosema ‘Wekeza kwa wanawake kwaajili ya maendeleo endelevu,” alisema Debora.

Debora alisema wanawake watakapofikiwa na taarifa za upimaji huo watoe taarifa ndani ya familia zao, kuwahamasisha watu waliopo katika familia zao ili kwapamoja waweza kupata fursa ya kupima moyo.

“Kambi kama hizi zinapofanyika zinampa mwananchi fursa ya kujijua, kupata matibabu kwa wakati, kwa muda mfupi na kwa gharama nafuu tofauti na mtu anayefika hospitali kwa kuchelewa,” alisema Debora.

Kaimu mkuu wa huduma za tiba wa Hospitali ya JKCI Dar Group Dkt. Eva Wakuganda akielezea huduma zitakazotolewa katika kambi maalumu ijulikanayo kama Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tiba mkoba katika kuadhimisha siku ya wanawake duniani. Kambi hiyo Machi 2 na 3, 2024 katika viwanja vya Hospitali ya JKCI Dar Group iliyopo Tazara jijini Dar es Salaam.

Mwakilishi wa umoja wa wanawake Hospitali ya JKCI Dar Group Debora Mkemwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kambi maalumu ijulikanayo kama Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tiba mkoba itakayofanyika Machi 2 na 3, 2024 katika viwanja vya Hospitali hiyo ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha siku ya wanawake duniani. Picha zote na Khamis Mussa


No comments