ZPC, CRDB ZAJADILI CHANGAMOTO CHA KIUCHUMI NA KIFEDHA
Meneja wa Biashara benki ya CRDB Zanzibar, Abdalla Duchi, akifafanua jambo wakati wamazungumzo baina ya viongozi wa benki hiyo na wa Klabu ya Wandishi wa Habari Zanzibar (ZPC) yaliyofanyika katika ofisi za benki hiyo zilizomo katika jengo la Michezani Mall, Zanzibar
Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
VYOMBO vya habari vimetakiwa kuwa
mstari wa mbele kuainisha changamoto za kiuchumi na kifedha zinazoikabili jamii
ili zipatiwe ufumbuzi na taasisi za kifedha.
Akizungumza katika kikao maalum na
uongozi wa Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC), Meneja wa Biashara wa Benki ya CRDB Zanzibar, Abdalla Duchi, alisema kuna changamoto ya uhaba wa
elimu ya kifedha katika jamii, jambo linalosababisha kuzorota kwa shughuli za
maendeleo.
Alieleza kuwa, pamoja na juhudi
zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuhimiza ujasiriamali na
uwezeshaji wa wananchi kiuchumi, bado elimu jumuishi ya kifedha inahitajika ili
kuwe na matokeo chanya.
Aidha, Duchi aliahidi kuendelea
kutumia vyombo vya habari na waandishi wa habari kueleza shughuli zinazofanywa
na benki hiyo, hivyo aliwataka wanahabari kuendelea kushirikiana nao kusambaza
elimu kwa umma.
“Niwapongeze kwa kazi kubwa
mnayoifanya ya kuelimisha jamii juu ya
masuala yanayohusu ustawi wao kiuchumi na kijamii, jambo linalopaswa kufanywa
kwa kasi zaidi kwa ushirikiano tunayoyaanzisha leo,” alieleza Duchi.
Alifafanua kuwa, benki hiyo ina huduma
mbalimbali zinazowagusa wananchi wa ngazi zote ikiwemo akaunti ya Kiislamu Al
Barakah na bima mbalimbali zinazoweza kuwanufaisha wateja pindi wanapopatwa na
majanga, misiba au ulemavu.
“Miongoni mwa bidhaa tulizonazo ni
bima ya mtu mmoja mmoja na ya vikundi ambayo hutoa mafao yasiyopungua shilingi
milioni moja kwa ajali, kifo, majanga, ulemavu wa kudumu, elimu na kadhalika
kwa gharama inayoanzia shilingi 1,000,” alieeleza meneja huyo.
Awali, Mwenyekiti wa ZPC, Abdallah Mfaume,
alieleza lengo la ziara hiyo inayofanyika kila mwanzo wa mwaka ni kuimarisha
mahusiano baina ya klabu na wadau wake.
Alieleza kuwa, ZPC ni taasisi mwamvuli
wa waandishi wa habari wanaoishi na kufanya kazi katika vyombo mbali vya habari
vya ndani na nje ya Zanzibar ikiwa na jukumu la kuwaunganisha kitaaluma ili
kujenga weledi wanachama wake kupitia shughuli mbalimbali.
Aliongeza kuwa, katika kutekeleza
majukumu yake, ZPC hutoa mafunzo yanayowajengea uwezo wanachama wake na
waandishi wa habari hivyo, kukua kwa mahusiano baina yake na benki hiyo
kutaongeza uelewa wa jamii na wanachama wa klabu juu ya masuala ya kifedha na njia
za kujiongezea kipato.
“Tumekuwa na utaratibu huu kila mwaka
lengo ni kukumbushana juu ya namna bora ya kufanya kazi pamoja kwa malengo ya
kukuza ufanisi wa malengo tuliyojiwekea kupitia shughuli za taasisi zetu,” alieleza Mfaume.
Kwa upande wake Meneja Biashara wa Benki ya Kiislamu wa CRDB Zanzibar, Anwar Said, alieleza kufurahishwa kwake na
ziara ya viongozi hao na kuongeza kuwa, benki hiyo inaendelea kutoa huduma mbalimbali kupitia akaunti ya Al Barakah tangu ilipoanzishwa Novemba 2021.
“Katika benki ya Kiislamu kuna huduma
na bidhaa nyingi sana ikilinganishwa na benki nyingine ambazo tutahitaji msaada
wa vyombo vya habari kuujulisha umma,” alieleza Anwar.
Katika ziara hiyo, Mfaume aliambatana na Katibu Mkuu wa ZPC, Mwinyimvua Nzukwi, Mjumbe wa Kamati Tendaji, Zuhura Msabaha na Mratibu, Mgeni Hamad, mbali ya Duchi na Anwar, CRDB iliwakilishwa na Afisa Biashara na Mauzo, Lucy Mbuya na Afisa Ubora wa huduma, Zainab Ally.
Meneja wa Biashara benki ya CRDB Zanzibar, Abdalla Duchi (kushoto) akizungumza na viongozi wa Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC), walipofanya ziara ya kukuza mahusiano katika ofisi za benki hiyo zilizomo katika jengo la Michezani Mall, Zanzibar.
No comments