JKCI YAFANYIKA KLINIKI YA MATIBABU YA MOYO MKOANI GEITA
Na Mwandishi Maalumu - Geita
WATAALAM wa afya wa
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wameweka kliniki maalumu ya matibabu ya
kibingwa ya magonjwa ya moyo kwa wagonjwa wanaohitaji huduma hiyo mkoani Geita.
Kliniki hiyo maalumu ya wiki moja imefanyika
katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato (CZRH) na kumalizika leo Februari 23,2024 kwa kufanywa
na wataalamu wa afya wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa CZRH ambapo wagonjwa
312 wamefanyiwa vipimo vya moyo na kupatiwa matibabu.
Kliniki hiyo inatarajiwa kufanyika
mara moja kila mwezi lengo likiwa kuwajengea uwezo wataalamu wa CZRH pamoja na
kuiwezesha Hospitali hiyo kutoa huduma za kibingwa za uchunguzi na matibabu ya
moyo kwa wagonjwa wa moyo waliopo kanda ya ziwa.
Akizungumzia kliniki hiyo Daktari
bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI) Williams Ramadhan alisema kati ya watu 312 waliopatiwa huduma watu 13
wamekutwa na matatizo ya kuziba kwa mishipa ya moyo, watu 12 wamekutwa na
matundu kwenye moyo, na watu 14 wamekutwa na matatizo ya umeme wa moyo
(arrhythmias).
“Watu 55 tumewakuta na tatizo la
shinikizo la juu la damu, watu saba wana magonjwa ya kuziba kwa mishipa ya damu
ya miguu, watu sita wana vidonda sugu kwasababu ya mishipa ya miguu kutanuka na
kuwa na shinikizo la juu la damu, na watu wawili tumewakuta na tatizo la
kutanuka kwa mshipa mkubwa wa aorta,” alisema Dkt. Ramadhan
Dkt. Ramadhan alisema wagonjwa 51
wamepewa rufaa kufika JKCI kwaajili ya matibabu zaidi ambapo 13 watahitaji
upasuaji wa kuzibua na kupandikiza mishipa ya damu, wagonjwa 14 watahitaji kufungwa
vifaa maalumu kurekebisha mfumo wa umeme wa moyo, wagonjwa 11 kufanyiwa
upasuaji wa mishipa ya miguu, wagonjwa 12 kufanyiwa upasuaji wa kuziba matundu
ya moyo na mgonjwa mmoja kupandikizwa mshipa mwingine wa bandia.
Kwa upande wake Mratibu wa huduma za
afya Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato (CZRH) Dkt. Osward Lyaba alisema
Hospitali hiyo ilianzisha kliniki ya magonjwa ya moyo miezi sita iliyopita
ambayo ilizinduliwa na aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) marehemu Prof. William Mahalu.
“Katika kuendeleza huduma za kliniki
hii wataalamu wa afya kutoka JKCI wameshirikiana nasi kwa kuweka kambi ya wiki
moja katika Hospitali yetu ikiwa ni sehemu ya kutujengea uwezo na kutoa huduma
kwa wagonjwa wa moyo wanaohitaji huduma za kibingwa,” alisema Dkt. Osward
Dkt. Osward alisema kambi hiyo
imehusisha wataalamu wa afya mabingwa wa matibabu ya moyo, mabingwa wa upasuaji
wa moyo na wataalamu wa vipimo vya magonjwa ya moyo.
"Mwitikio umekuwa mkubwa kwani kwa
siku tatu za mwanzo tumeweza kuona takribani watu 230 waliojitokeza kufanyiwa
uchunguzi na kupatiwa matibabu ya moyo na wale waliohitaji huduma zaidi
wamepewa rufaa kufika JKCI kwaajili ya matibabu zaidi,” alisema Osward.
Fundi sanifu wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Jasmine Keria akimpima kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiography – ECHO) mkazi wa Geita aliyefika katika kliniki maalumu ya siku tano ya uchunguzi na matibabu ya moyo iliyofanywa na wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato (CZRH) iliyopo mkoani Geita.
wakazi wa Geita wakiwa katika foleni
ya kusubiri kupata huduma katika kliniki maalumu ya siku tano ya uchunguzi na
matibabu ya moyo iliyofanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Chato (CZRH)
iliyopo mkoani Geita. Jumla ya wagonjwa 312 wamepata huduma ya uchunguzi na
matibabu katika kliniki hiyo iliyomalizika Februari 23,2024.
No comments