Header Ads

ad

Breaking News

Yanga yamshitaki Akrama TFF




UONGOZI wa klabu ya Yanga, umemlalamikia mwamuzi wa mchezo wao dhidi ya Simba, Mathew Akrama, na kulitaka Shirikiso la Soka Tanzania (TFF), kuipitia upya mechi hiyo iliyochezwa Oktoba 3, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, ili waangalie madudu yaliyofanywa na mwamuzi huyo.

Yanga wamemlalamikia mwamuzi Akrama na wasaidizi wake, Samuel Mpenzu kutoka Arusha na Ephrony Ndissa wa Dar es Salaa, kuwa walishindwa kutafsiri sheria 17 za soka.

Akizungumza jana katika makao makuu ya klabu hiyo, mitaa ya Jangwani na Twiga, Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Lawrence Mwalusako, alisema mwamuzi huo alikuwa akipendelea sana upande mmoja, na kusababisha kutoa maamuzi yasiyo sahihi.

Mwalusako alisema kuwa, hata katika utoaji wa kadi kwa wachezaji, alikuwa akipendelea sana wachezaji wa Simba, kwani makosa aliyofanya Haruna Moshi ‘Boban’, hayakustahili kupewa kadi ya njano.

“Mwamuzi aliipendelea sana Simba, ile mechi kila mmoja aliiona na makosa yaliyofanywa na Boban, pia yalionekana dhahiri, lakini mwamuzi akampa kadi ya njano,” alisema Mwalusako.
Alisema kuwa, TFF inapaswa kuiangalia mechi ile upya na kuitolea maamuzi dhidi ya mwamuzi Akrama, kwa kile alichokifanya, kwani kila aliyeishuhudia aliona makosa yaliyokuwa yakifanyika.

Alisema kuwa, mbali na mwamuzi huyo wa kati, hata wasaidizi wake walikuwa wakitoa maamuzi ya kuiuufaisha upande mmoja.

Katika mchezo huo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliochezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, timu hizo zilitoka sare ya bao 1-1.

No comments