Header Ads

ad

Breaking News

Simba yabanwa na Kagera Sugar U/Taifa, zatoka 2-2


Kikosi cha Simba

KWELI Kagera Sugar ni kiboko ya vigogo! Mabingwa wa soka nchini, Simba, jana walishindwa kutamba baada ya kubanwa na Wakata Miwa wa Kagera, na kutoka nao sare ya mabao 2-2, katika mechi iliyopigwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

 Majigambo ya Kocha Mkuu wa Kagera Sugar, Abdallah Kibaden ‘King Mputu’, yalikuwa ya kweli baada ya vijana wake kuonesha soka zuri na la kuvutia, huku wakitoka nyuma na kufanikiwa kusawazisha mabao yote mawili.

Katika mechi hiyo, Simba walianza kwa kasi na kulisakama lango la wa Kagera Sugar, ambapo dakika ya nane, Felix Sunzu akishindwa kuunganisha kwa kichwa mpira.

Dakika ya tisa, Sunzu alirekebisha makosa yake, kwa kufunga bao kwa kichwa akiunganisha mpira uliopigwa na Mrisho Ngassa, aliyewashinda ujanja mabeki wa Kagera Sugar.

Sunzu alikuwa akiisumbua ngome ya wapinzani wao, lakini alishindwa kuiongezea bao timu yake ya Simba, baada ya kuunganisha kwa kichwa mpira wa krosi uliotoka kwa Said Nassoro ‘Cholo’, na kutoka nje ya lango la Kagera Sugar.

Kagera Sugar walizinduka na dakika ya 26, Daud Jumanne, alishindwa kuunganisha vizuri mpira uliopigwa na George Kavila na kutoka nje ya lango la Simba.

Simba walifanya shambulizi la nguvu dakika ya 29, baada ya beki Juma Nyosso kuonana vizuri na Mwinyi Kazimoto, lakini mpira aliopiga ulitoka nje ya lango la wapinzani wao.

Wakizidi kuliandamaa lango la wapinzani wao, Simba, Ngassa na Haruna Moshi ‘Boban’, walipata nafasi nzuri, lakini walishindwa kuifungia timu yao bao.

Pamoja na mashambulizi hayo, Kagera Sugar, walijitutumua na kuliandama lango la wapinzani wao, ambapo dakika ya 43, Shija Mkina, alikosa bao la wazi.

Ngassa aliwainua mashabiki wa Simba dakika ya 51, baada ya kutumia vizuri makosa ya beki wa Kagera Sugar, Martin Muganyizi, bao ambalo liliwafanya wachezaji wa Kagera kumfuata mwamuzi msaidizi namba moja, Julius Kasitu kutoka Shinyanga aliyenyoosha juu kibendera, huku mwamuzi wa kati Ronald Swai kutoka Arusha, akishindwa kumwangalia.

Mbaya wa Yanga, Them Felix, alithibitisha ubora wake wa kuzifumania nyavu, baada ya kuifungia timu yake ya Kagera Sugar bao dakika ya 65, kwa kichwa.

Wakiwa na nguvu mpya, Kagera Sugar walilisakama lango la Simba na kufanikiwa kupata penalti baada ya Nyosso kumchezea vibaya Paul Ngwai, penalti iliyotumbukizwa wavuni na Salum Kanoni.

Felix aliingia uwanjani kuchukua nafasi ya Darlington Enyima, dakika ya 53, lakini dakika mbili baadaye akamchunulia Juma Kaseja na kumpeleka nyavuni kuokota mpira ukiwa tayari umezitikisa.
 
Simba: Juma Kaseja, Said Nassoro ‘Cholo’, Amir Maftah, Juma Nyoso, Pascal Ochieng, Mwinyi Kazimoto, Mrisho Ngassa, Amri Kiemba, Felix Sunzu, Haruna Moshi ‘Boban’, Emmanuel Okwi.
Kagera: Andrew Ntalla, Salum Kanoni, Martin Muganyizi, Amandus Nesta, Benjamin Effe, Malagesi Mwangwa, Daud Jumanne, George Kavilla, Shija Mkina, Darlington Enyima, Wilfred Ammeh.

Katika mechi ya utangulizi, Simba B iliichapa Ruvu B, mabao 3-0, katika mechi ya kirafiki iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Mabao ya Simba B yalifungwa na Ramadhan Salum dakika ya 65 na 70, ambapo bao la tatu likipachikwa wavuni na Miraj Athuman dakika ya 85.

No comments