Header Ads

ad

Breaking News

Yanga yaua Taifa, yaichapa JKT Ruvu 4-1




Na Mwandishi Wetuu

YANGA jana ilizinduka katika Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya kuichapa JKT Ruvu mabao 4-1 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Katika mechi ya kwanza ya ligi hiyo, mabingwa hao wa Afrika Mashariki na Kati waliambulia suluhu ugenini dhidi ya Prisons Mbeya, kabla ya kulala kwa mabao 3-0 dhidi ya Mtibwa Sugar mjini Morogoro katikati ya wiki.

Na ikicheza bila Kocha Mkuu, Tom Saintfiet aliyetimuliwa juzi, Yanga iliuanza mchezo huo wa jana kwa kasi ya ajabu na kufanikiwa kupata bao la kwanza dakika ya tano kupitia kwa nahodha wake, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, akipokea krosi ya Athuman Idd ‘Chuji’, aliyepokea mpira wa adhabu kutoka kwa Haruna Niyonzima.

Adhabu hiyo ilitokan na Simon Msuva kuangushwa na Damas Makwaya nje kidogo ya eneo la hatari.

Bao la pili la Yanga lilifungwa na Didier Kavumbagu katika dakika ya 32 kutokana na kazi nzuri iliyofanywa na beki wa kushoto Oscar Joshua.

Katika kipindi cha pili, Yanga waliendeleza kasi yao na kupata bao la tatu kupitia kwa Msuva kutokana na uzembe wa mabeki wa JKT Ruvu kushindwa kuondoa mpira katika eneo la hatari.

Kavumbagu alifunga hesabu ya mabao ya Yanga baada ya kuifungia timu yake hiyo bao la nne kutokana na makosa ya kipa wa JKT Ruvu ambaye aliutema mpira alioudaka kutokana na shuti kali la Joshua.

JKT Ruvu walipata bao la kufutia machozi kupitia kwa Credo Mwaipopo, ikiwa ni baada ya Joshua kufanya makosa yaliyotumiwa vyema na Hussein Bunu aliyeinasa pasi ya kizembe ya beki huyo na kumpasia mfungaji, hiyo ikiwa ni dakika ya 68.

Baada ya bao hilo, JKT Ruvu walionekana kucharuka na kufanya mashambulizi ya nguvu langoni mwa Yanga, lakini kipa wa timu hiyo, Yaw Berko, alikuwa imara kuokoa michomo yote iliyoelekezwa langoni mwake.

Katika mchezo mwingine wa ligi hiyo uliochezwa kwenye Uwanja wa Chamazi, Azam iliichapa Mtibwa Sugar bao 1-0, bao lililowekwa kimiani na Kipre Tchetche dakika ya 29.

No comments