Header Ads

ad

Breaking News

Ngassa ni mwisho wa matatizo, apiga bao la ushindi Simba


Mrisho Ngassa (kushoto), wa Simba, akiwatoka mabeki wa Tanzania Prisons, Laurian Mpalile (wa pili kushoto) na David Mwantika, wakati wa mechi ya Ligi Kuu Tanzania Bara iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, leo. Simba ilishinda mabao 2-1. Picha na www.fullshangweblog.com


MSHAMBULIAJI wa pembeni wa timu ya Simba, Mrisho Ngassa, amezidi kuzitendea haki fedha za usajili zilizotolewa na klabu hiyo, kwa kuonesha kiwango cha hali juu, huku akichangia sehemu kubwa ya ushindi wa timu hiyo dhidi ya Tanzania Prisons wa mabao 2-1 .

Katika mechi zote alizocheza, Ngassa amekuwa chachu ya ushindi kwa kufunga ama kutoa pasi za mwisho za mabao ya timu yake, ambapo jana aliifungia timu yake bao la pili lililowapa ushindi katika mchezo huo uliopigwa Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Katika mechi ya leo, Ngassa alikuwa akiwasumbua mabeki wa Prisons ya Mbeya, ambayo imerejea Ligi Kuu Bara, baada ya kushuka daraja miaka, huku akitoa pasi za mwisho, ambapo mojawapo ikiwa kwa Ramadhan Chombo ‘Redondo’, aliyebaki na kipa David Abdallah, aliyeokoa kwa miguu.

Mbali na Ngassa, Prisons katika mchezo huo uliokuwa wa kuvutia huku timu zote zikishambulia, ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya sita, lililofungwa na Lugano Mwangama kwa shuti kali, aliloshindwa kudaka kipa wa Simba, Juma Kaseja.

Kazi nzuri iliyofanywa na Mwinyi Kazimoto kumsukumia pasi nzuri Amir Maftah, ilizaa bao baada ya beki huyo wa kushoto kutoa pasi safi iliyomkuta Mzambia Felix Sunzu na kuisawazishia timu yake bao hilo.
Bao hilo liliwaongezea nguvu Simba, ambapo dakika ya 48,  Sunzu alishindwa kuunganisha vizuri kwa kichwa, mpira wa krosi uliopigwa na Ngassa na kutoka nje.

Ngassa akidhihirisha ubora wa kiwango chake, aliwainua mashabiki wa Simba, baada ya kuifungia timu yake bao la pili dakika ya 55, kwa shuti kali lililompita kipa Abdallah, aliyejaribu kuudaka na kushuhudia nyavu zake zikitikisika.  

Katika mchezo huo, beki wa kushoto wa Simba, Amir Maftah alitolewa nje dakika ya 81, kwa kuonesha kadi nyekundu na mwamuzi Paul Soleji kutoka Mwanza, baada ya kumchezea vibaya wa Khalid Fupi wa Tanzania Prisons.

Simba, lkwa matokeo hayo imerejea kileleni mwa ligi hiyo, baada ya kushinda mechi zote nne, ikiwa na pointi 12, ikifuatiwa na azam FC iliyojikusanyia pointi tisa, huku Coastal Union wakiwa na pointi nane.

Simba: Juma Kaseja, Nassoro Masoud ‘Cholo’, Amir Maftah, Shomari Kapombe, Juma Nyosso, Mwinyi Kazimoto, Amri Kiemba, Ramadhan Chombo ‘Redondo’, Edward Christopher, Felix Sunzu, Mrisho Ngassa.

Prisons: David Abdallah, Aziz Sibo, Laurian Mpalile, Lugano Mwangama, David Mwantika, Khalid Fupi, Misango Magai, Fred Chudu, Elias Maguri, Peter Michael,John Matei.


No comments