Header Ads

ad

Breaking News

Ngassa aigomea Azam



BAADA ya Simba na Yanga kuvutana juu ya mshambuliaji wa Azam FC, Mrisho Nggasa, hatimaye jana ametua kwa Wekundu wa Msimbazi, Simba SC,  kwa mkopo.

Ngassa ambaye alionesha mapenzi ya wazi ya kutaka kwenda Yanga, lakini uongozi wa Azam FC uliamua kutoa ofa kwa mchezaji huyo kwa timu yoyote itakayokuwa ikimtaka.

Baada ya kutoa hofa hiyo, timu za Simba na Yanga zilituma maombi katika timu yake ya Azam FC, lakini jana, Simba walifanikiwa kumnasa kwa mkopo wa ada ya sh. milioni 25.

Akizungumza na gazeti hili jana, Ofisa wa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga,  alisema kwamba, wamefanikiwa kumnasa Nggasa kwa mkopo.

“Tayari tumemalizana na Azam FC, tumemchukua kwa mkopo, tutamwangalia hadi Desemba mwaka huu, kama atafanya vizuri, tutamsajili moja kwa moja kwa kutumia ada itakayolipwa na timu ambayo Emmanuel Okwi anafanya majaribio,”,” alisema Kamwaga.

SuperStar ilimtafuta Meneja wa Azam FC, Patrick Kahemele, ili kujua ukweli wa habari hizo, ambapo alikiri na kusema kuwa, wamemtoa kwa mkopo Simba.

“Ni kweli tumemtoa kwa mkopo Simba,  wametulipa sh. milioni 20, na watakuwa wanamlipa mshahara wenyewe,” alisema.

Alipoulizwa kama mshambuliaji huyo alishirikishwa kwenye vikao vyao vya kujadiliana uhamisho wake, alisema kuwa, hakushirikishwa, lakini atapewa taarifa ya maandishi.

“Yeye ni mchezaji, tumeamua kumpeleka Simba bila ya kumshirikisha, huu ni kama uhamisho kutoka kituo kimoja kwenda kingine,” alisema.

“Ninapozungumza na wewe, tunamwandikia barua ya kumweleza maamuzi yetu,” alisema.
Wakati huohuo, baba mzazi wa Mrisho, Khalfan Ngassa, alisema kuwa, mtoto wake alimpigia simu ya kumtaka ushauri kuhusu uhamisho huo.

Mrisho alimweleza baba yake kuwa, amepata taarifa ya ujumbe mfupi wa simu, kuwa amepelekwa Simba kwa mkopo bila ya kushirikishwa.

Baba yake alimuuliza kama alishirikishwa kwenye mpango huo wa uhamisho, ambapo Mrisho alijibu kuwa, hakushirikishwa.

“Mimi nimeambiwa kwa ujumbe mfupi wa maneno kwenye simu, sikushirikishwa katika suala hilo, lakini malengo yangu ni kurudi Yanga,” alisema.

Baba yake alimtaka mtoto wake huyo kuendelea na malengo yake, kwani tayari alikuwa na mtandao mkubwa wa marafiki ndani na nje ya uwanja.

Mzee Ngassa alisema: “Nimemshauri kurejea katika timu yake ya zamani ambayo amezoeana na kila mmoja mpaka viongozi, kama akienda Simba ataanza kazi upya ya kujenga mahusiano ya ndani na nje ya uwanja,” alisema.

No comments