Header Ads

ad

Breaking News

Yanga, Simba vitani kumwania Ngassa



USAJILI wa kiungo mshambuliaji wa Azam FC, Mrisho Ngassa, umeendelea kuwa wa simtofahamu, baada ya kuzuka kwa vita ya kumwania nyota huyo kati ya klabu za Simba na Yanga, ambazo zote zineonesha nia ya kumsajili kwa ajili ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara.

Uchunguzi wa kina uliofanywa na SuperStar umeonesha kwamba, timu zote hizo mbili zinazopatikana katika Jiji la Dar es Salaam, zimekuwa kwenye harakati kubwa za kumsajili nyota huyo ambaye aliwahi kuwika na klabu za Toto Africans na Kagera Sugar katika miaka ya nyuma.

Imebainika kwamba, Yanga ndio walikuwa wa kwanza kufanya mazungumzo ya mdomo na baadaye maandishi kwa njia ya barua pepe (email), ili kufanikisha usajili wa nyota huyo.

Kati ya watu waliohusika na mazungumzo hayo ni Katibu Mkuu wa Yanga, Mwesigwa Selestine, ambaye alituma barua pepe juzi kwenda kwa Meneja wa Azam FC, Patrick Kahemele, lakini siku  hiyo hiyo Simba nao walitua Azam FC kwa nia ya kumsajili nyota huyo.

Katika kile kilichoonekana kuwa ni vita kwa pande zote mbili, Mwenyekiti wa kamati ya usajili wa Klabu ya Yanga, Seif Ahmed ‘Magari’ alifanya mazungumzo na Mmiliki wa Azam, Yusuf Bakhressa na kuanisha kile walichonacho.

Katika kujua ukweli, SuperStar ilimtafuta, Katibu Mkuu wa Azam Idrissa Nassor ambaye alikiri kuwepo kwa mazungumzo ya mwisho kati ya Azam na Simba, ambayo ilionesha nia ya kumsajili Ngassa.

“Suala hili hatutaki kulifanyia mzaha wala kuwa na kificho, Simba wamekuja na wametoa ofa yao, lakini Yanga hadi sasa hawajafika, hivyo tunazungumza na mtu aliye mezani na dakika chache zijazo tutakuwa tumeafikiana na Simba.

“Mtoto ameonesha mapenzi ya kwenda Yanga, na sisi tumetoa ofa, lakini cha ajabu hadi sasa Yanga wamekaa kimya, kwa hiyo hatuwezi kuwalazimisha,” alisema Nassor ikiwa ni muda mfupi kabla ya kwenda kufuru.

Kutokana na utata huo, SuperStar ilipiga hodi katika kamati ya usajili ya Yanga, ambapo ilikutana na Mwenyekiti wa kamati hiyo, Seif Magari ambaye alikiri kufanya mazungumzo na Bakhressa juu  ya usajili wa Ngassa na kukubaliana baadhi ya mambo muhimu yanayoweza kukamilisha jambo hilo.

“Kweli jana (juzi) usiku nilizungumza na Bakhressa, nikamweleza kile tulichonacho. Moja ya ofa tulizotoa ni kupewa kwa mkopo au wakubaliane na dau tulilotoa maana kijana ameonesha nia na mapenzi kwa Yanga.

“Katika mazingira haya, ni wazi kuwa kama kuna mipango ya kumpeleka Simba, waseme ila tunajua kuwa, hilo haliwezekani, kwani ikumbukwe kuwa, Azam FC nao wameamua kuuza, baada ya kuonesha mapenzi ya kucheza Yanga, je? iweje apelekwe Simba,  kama alishindwa Azam tusiokuwa na upinzani nao, ataweza kucheza Simba?

“Kwa busara namshauri Idrissa asikurupuke kuzungumza na vyombo vya habari, ila afanye mawasiliano na bosi wake (Bakhressa), kwa sababu tatizo ninaloliona Azam kila mtu ni kiongozi,” alihoji Magari.

Kwa hali hiyo, uchunguzi wetu unaonesha kwamba, ndani ya Azam kuna tatizo la mawasiliano ambalo limesababisha kuwepo kwa mgongano baina ya viongozi wake wa juu.

Katika mechi ya nusu fainali kati ya Azam na AS Vita Club ya DR Congo, Ngassa alifunga bao la ushindi na kuibusu jezi ya Yanga, ambapo mashabiki walimpa jezi hiyo na kuivaa, hali iliyozusha maswali mengi.

Nyota huyo aliwahi kuzitumikia klabu za Toto Africans ya jijini Mwanza na baadaye aliunga na Kagera Sugar  kisha kutua Yanga ambapo Azam ilimsajili kwa kitita cha  zaidi ya sh milioni 50.

ciao

No comments