Header Ads

ad

Breaking News

Sounders FC kushirikiana na Tanzania


Msafara wa Waziri wa Maliasi na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki (katikati), ukiwa pamoja na wenyeji wao wa Seattle Sounders FC/Seattle Seahawks, kwenye uwanja wa klabu hiyo mjini Renton, Washington, Marekani, hivi karibuni. Tanzania na Seatle zimekubaliana kushirikiana katika sekta mbalimbali.
 Na Mwandishi Wetu, Washington

TIMU ya Seattle Sounders FC ya Marekani imetangaza ushirikiano na Tanzania, nchi ambayo ni nchi kubwa kabisa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Ushirikiano huo ulitiwa saini na Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Hamis Kagasheki (Mbunge) na Mmiliki wa timu ya Seattle Sounders, Joe Roth,  katika hafla fupi iliyofanyika jana mjini Renton.

Mbali ya Waziri Kagasheki, wengine walioshuhudia kutiwa saini kwa ushirikiano huo ni Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Mwanaidi Maajar, Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Utalii Tanzania Dr. Aloyce Nzuki  na maofisa wengine kutoka Wizara ya Utalii, ubalozi na maofisa wa Seattle Sounders FC.

Mambo muhimu katika ushirikiano huo ni uwekwaji wa alama za vivutio vya utalii vya Tanzania katika maeneo mbalimbali kama CenturyLink Field na Starfire Sports Complex,  uwanja wa mazoezi wa Sounders FC uliopo eneo la Tukwila.

Vivutio vya Utalii wa Tanzania vitakavyowekwa katika maeneo hayo ni picha za Mlima Kilimanjaro, hifadhi za Serengeti, Ngorongoro Crater na Zanzibar.

"Ushirikiano wetu na Bodi ya Utalii Tanzania (TTB),  utasaidia kutangaza vivutio vya Utalii vya Tanzania nje ya mipaka yake, kwani kuna vivutio vya ajabu na kuleta unafuu kwa watalii ,” alisema mmiliki wa timu ya Sounders FC,  na kuongeza kuwa, ushirikiano huo utatoa nafasi muhimu kwa  soko la utalii wa nchini.

Waziri Kagasheki mbali ya kupongeza kwa kufanikisha hatua hiyo muhimu katika sekta ya Utalii nchini, alisema ushirikiano huo utatoa fursa nyingi kwa watanzania na wamerekani kwani utaimarisha juhudi za Wizara ya Utalii katika kukuza soko la utalii wa kimataifa na wa ndani.

Kagasheki pia alisema ushirikiano huo utatoa fursa za kibiashara kwa nchi zote mbili na kuongeza uwekezaji.

Katika kuhakikisha zoezi la ujumbe wa kupromoti vivutio vya utalii wa Tanzania vinawafikia wengi, michoro mbalimbali ya ukutani itachorwa ndani ya uwanja upande wa kaskazini magharibi na kaskazini mashariki  na itaonekana kwa mara ya kwanza  kwenye televisheni nchini Marekani, wakati wa mechi ya Sounders FC dhidi ya Chelsea kwenye Uwanja wa Field CenturyLink Julai 18, wakati Tanzania itakuwa Julai 19.

Pia, maofisa wa TTB watakuwa mbele wakati wa mkutano wa kabla ya mechi na mashabiki wa soka  na kuzungumzia masuala mbalimbali ya utalii na usafiri katika nchi yao.

Seattle Sounders FC ilianza majadiliano ya ushirikiano na Tanzania mwaka 2010, ambapo Kocha msaidizi wa timu hiyo, Kurt Schmid, alikuja nchini katika mpango wa kutafuta vipaji vya wachezaji.

Mchezaji wa timu ya Taifa, Mrisho Ngassa, wa Azam FC, alisafiri mpaka Marekani na kucheza mechi ya kihistoria kati ya Seattle Sounders na Machester United mwaka jana.

No comments